Friday 24 August 2012

Dk. Slaa: CCM wana sababu za kikoloni

 
KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA ), Dk. Willibrod Slaa, amesema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinachukiwa na wananchi kutokana na kuendelea kujitetea kwa kutumia sababu zilizotumiwa na wapigania uhuru wa Tanganyika kujikomboa katika mikono ya wakoloni.

Akizungumza katika mikutano ya hadhara kwenye vijiji mbalimbali vya kata za Ngerengere na Makambarai, Dk. Slaa alisema serikali ya CCM imeshindwa kutengeneza fursa ya wananchi kujiletea maendeleo yao licha ya kuwa katika nchi yenye rasilimali nyingi.

“Mwalimu Nyerere pamoja na wapigania uhuru wengine wa Tanganyika hawakumkataa mkoloni kwa sababu ya rangi, dini wala hali zao isipokuwa waliwakataa kwa vile walishindwa kuwaondolea watu umaskini, ujinga na maradhi ambayo yanaendelea kutuandama kila wakati,” alisema.

Alisema kuwa hayati Mwalimu Nyerere alifikia malengo kwa kuonesha njia ya kupita, hivyo waliomfuatia walikuwa na wajibu wa kuhakikisha njia hiyo inapitika lakini serikali ya CCM imeamua kuziba njia hiyo.

Huku akisoma takwimu za maendeleo katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, linaloongozwa na Dk. Lucy Nkya (CCM), Dk. Slaa alisema kuwa hakuna sababu ya kuendelea kukivumilia chama hicho kwa sababu ya kufanana kwa rangi na badala yake wananchi wanapaswa kuchukua hatua ya kukipumzisha.

“Kila mmoja hapa amesikia takwimu nilizosoma, tena zinatokana na vitabu vya serikali yenu hii mliyoichagua na kuiweka madarakani, mlichagua rais wa CCM, mbunge wa CCM, Diwani wa CCM, mwenyekiti wa kijiji na serikali ya kijiji ya CCM, sasa nawasomea hapa ufisadi unaofaywa mnaanza kusikitika,” alisema.

Alisema ni aibu miaka 50 baada ya Uhuru kusikia Watanzania wakizungumzia upungufu wa madawati wakati nchi nyingine zikiwa zinashindana kwenda kuangalia uwezekano wa kufanya utafiti utakaozisaidia nchi zao.


No comments:

Post a Comment

Chadema UK Ndani ya Milton Keynes

DAR NI SISI - VIDEO MAISHA YA WANADAR HATA BAADA YA MIAKA50 YA UHURU